Wednesday, May 8, 2013

RECHO AFURAHIA KUSHIRIKI TUZO ZA KILI KWA MARA YA KWANZA

MSANII maarufu wa  muziki kutoka nyumba ya sanaa tanzania(THT) Winfrida Josephat 'Recho' amefurahi baada ya kuingia katika vinyang'anyiro vya Tuzo za Kilimanjaro katika vipengele vitatu.
Akizungumza na Keshe BlogSpot jijini Dar es salaam, Recho alisema anafuraha  baada ya kuingia katika vinyang'anyiro 3 ikiwemo kile cha cha msanii bora wa kike wa mwaka kwa mwaka jana ambacho kinakutanisha wasanii waliofanya vizuri na wengi wakiwa ni wasanii wakongwe.
Recho alisema katika kipengele hicho anachuana na wasanii wenye majina makubwa na wenye uwezo mkubwa katika tasnia ya muziki hivyo kwake hiyo ni faraja tosha na anaamini waandaaji waliona kazi nzuri alizofanya mwaka jana na hiyo ndiyo sababu ya yeye kuchaguliwa.

"Nikizungumzia upande wa msanii wa bora wa kike kwa mwaka jana ninachuana na Khadija Kopa,Isha Mashauzi,Lady Jay Dee pamoja na Mwansiti hivyo ninategemea kuwa na ushindani mkubwa lakini pia ninaamini ninastahili ndio sababu nimekua mmoja wao" Alisema Recho.
Nyota huyo mwenye sauti na muonekano sawa na Ray C alisema anaamini maisha yake yapo kwenye muziki na mafanikio machache aliyonayo ikiwemo kujitegemea mwenyewe na kuweza kusaidia familia yake tofauti na awali huo ni mwanzo wa safari na kupitia juhudi zake anawaahidi mambo makubwa mashabiki wake.
Recho alisema anawaomba watanzania wampigie kura kwa wingi ili aweze kushinda Tuzo hizo zenye heshima kubwa kwa wasanii hapa nchini na kushinda ni moja kati ya hatua za maendelea yake yakimuziki ambapo analenga kufanya kazi ya kimataifa zaidi ili aweze kutangaza muziki Tanzania duniani kote.
Recho ni msanii anayewania tuzo katika kipengele cha msanii bora wa kike wa mwaka,msanii bora wa kike wa bongo fleva na nyimbo bora ya zouk ambayo ni nashukuru umerudi.Tuzo za Kilimajaro Music ni tuzo zinazotolewa kwa wasanii walifanya vizuri kila mwaka.
.



 

No comments:

Post a Comment